Tuesday, April 14, 2009

Mama Salma Kikwete awataka wananchi visiwani zanzibar kutokuogopa kukopa fedha benki

Mke wa Rais Mama Salma Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa Taasisi ya Wanawake na Maendeleo(WAMA) amewataka wananchi visiwani Zanzibar kutokuogopa kukopa fedha Benki au katika asasi za fedha ili waweze kuongeza mitaji nahivyo kujikwamua na hali ngumu ya maisha.

Mama Salma aliyasema hayo leo wakati akifungua mkutano mkuu wa siku moja wa Chama cha Akiba na Kukopa (SACCOS) ya Melinne uliofanyika katika chuo cha Karume Mbweni visiwani Zanzibar.

“Madhumuni ya mkutano huu pamoja na mambo mengine ni kufanya uchaguzi mkuu wa viongozi wapya wa kuwaongoza katika kipindi kinachofuata”“Wosia wangu katika hili ni kuwapima wanachama wenu wanaogombea kwa uwezo, imani na uaminifu wao kama vile mlivyofanya kwa viongozi waliotangulia. Wapimeni viongozi kwa vigezo vya uongozi na si vinginevyo”, alisema.

Akimkaribisha mgeni rasmi Waziri Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Shamsi Vuai Nahodha ambaye pia ni Mwakilishi wa jimbo la Mwanakwerekwe na ni mlezi wa SACCOS hiyo alisema kuwa SACCOS hiyo ni moja ya SACCOS imara visiwani Zanzibar.“Kinababa si watu wazuri sana katika suala la utunzaji wa fedha ukiwapa kutunza fedha zinaweza kupotea katika mazingira yasiyoeleweka ila kina mama ni wasimamizi na wachumi wazuri sana katika jamii”.

“Nawashauri msifanye makosa ya kuchagua viongozi wengi wanaume kwa kufanya hivyo SACCOS yenu inaweza kuyumba ili kuinusuru ni heri kama mmeridhika na uongozi wa viongozi waliopita muwachague haohao waendelee kuongoza”, alisemaAkisoma risala ya chama hicho Ahmada Hassan ambaye ni mjumbe alisema kuwa wamekuwa tukifuatilia sana SACCOS za Tanzania bara na kuona hatua mbalimbali za maendeleo walizofikia na kujiuliza kwa nini bara waweze na wao washindwe?

“Tunatoa ahadi iwapo tutaweza kukabiliana na changamoto hizi tunaamini kuwa ifikapo mwaka 2013 SACCOS yetu itakuwa ni Benki ya wananchi”, alisema. Wanachama 620 waliooomba mikopo wamepatiwa kwa kipindi cha miaka mitatu na jumla ya fedha zilizokopeshwa ni zaidi ya milioni mia nne ambapo asilimia kubwa ya waliokopa ni wanawake wanaofanya biashara ndogondogo.

SACCOS hiyo ilianza mwaka 2005 ikiwa na wanachama 150 wanawake wakiwa 123 na wanaume 27 hadi sasa kuna jumla ya wanachama 920 wanawake wakiwa 677 na wanaume 243.

Msomaji
Zanzibar

No comments: