Thursday, August 27, 2009

SERIKALI YAKANUSHA MADAI YA TBC KUUZWA

Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo MH. George Mkuchika akizungumza wakati wa mkutano na waandishi wa habari jijini Dar es salaam.


Serikali imekanusha madai ya shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) kuuzwa kinyemela kama ilivyoonyeshwa katika taarifa iliyotolewa na chombo kimoja cha habari hapa nchini.Kauli hiyo imetolewa leo jijini Dar esa Salaam na Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo George Mkuchika wakati wa mkutano na waandishi wa habari kuhusu hatua iliyochukuliwa na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) kuunda kampuni mpya iitwayo Star Media (Tanzania) Limited kwa ubia na mwekezaji.

Amesema Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) kama shirika la umma halijauzwa na kuwataka wananchi kutoamini taarifa zozote zinazotolewa kuhusu kuuzwa kwa namna yoyote kwa shirika hilo.

“ Nawathibitishieni leo kuwa shirika la Utangazaji (TBC) halijauzwa ,bado ni la wananchi na kamwe halitauzwa” amesisitiza.Ameongeza kuwa TBC ni mali ya umma na itaendelea kuwa hivyo kama shirika la umma linalomilikiwa na serikali kwa asilimia 100 na kuongeza kuwa Star Media Tanzania Limited ni Kampuni tanzu ya TBC.

Amefafanua kuwa TBC imeunda kampuni hiyo mpya kwa ubia na mwekezaji aliyeteuliwa kihalali ili kutekeleza mabadiliko ya Digitali na kuendesha mitambo ya kurushia matangazo yake nchi nzima kazi ambayo itakamilika mwaka 2012 kwa gharama ambazo TBC isingeweza kuzimudu yenyewe kutokana na jukumu hilo kuhitaji utaalam mkubwa wa kiufundi ili kukamilisha ufanisi.

Msomaji
Dar es salaam

No comments: