Monday, March 12, 2012

MKAPA KUONGOZA UZINDUZI WA KAMPENI ARUMERU





Wajumbe wa kamati kuu CCM wakiongozwa na Rais Jakaya Kikwete wakati wa kupitisha jina la Sioi Sumari kugombea jimbo la Arumeru
























RAIS Mstaafu, Benjamin Mkapa leo anatarajiwa kuongoza uzinduzi wa kampeni za CCM za uchaguzi mdogo wa ubunge Arumeru Mashariki zitakazofanyika katika Kata ya Usa River, wilayani Meru, Arusha.

Uzinduzi wa kampeni za CCM unakuja siku moja tangu wapinzani wao wakuu, Chadema wazindue kampeni katika Uwanja wa Leganga, Usa River wakiongozwa na Mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe.

Vyama hivyo viwili vyenye upinzani mkubwa nchini, vinatarajiwa kubeba ajenda mbili kuu; migogoro ya ardhi na uhaba wa upatikanaji maji kwa matumizi ya nyumbani na kilimo.

Baadhi ya wakazi wa Arumeru wanasema mbunge wanayemtaka ni yule atakayeweza kuwaondoa katika migogoro ya ardhi ambayo inachochewa na maeneo makubwa kuchukuliwa na wawekezaji.

Katibu wa CCM Mkoa wa Arusha, Mary Chatanda aliwaambia waandishi wa habari jana kwamba viongozi mbalimbali wa kitaifa watakuwa na vikao vya ndani katika kata zote 17 za jimbo hilo.

“Tayari tumekutana na makundi yote na sasa hali ni shwari. Makundi yote yameungana kumuunga mkono mgombea wetu Siyoi Sumari ambaye tuna uhakika atashinda,” alisema Chatanda.

Awali, kulikuwa na utata kama Rais mstaafu huyo, atafika kuzindua kampeni hasa kutokana na mpasuko mkubwa wa viongozi uliotokana na kura za maoni na makundi ya wanaojipanga kuwania urais mwaka 2015.

Alisema uzinduzi huo utahudhuriwa na viongozi kadhaa, akiwemo Katibu Mkuu wa CCM, Wilson Mukama na Mlezi wa chama hicho Mkoa wa Arusha, Stephen Wassira... “Kabla ya uzinduzi ambao utaanza majira ya saa 9:00 alasiri, kutakuwa na maandamano ya wafuasi wa CCM kutoka nyumbani kwa mgombea wetu eneo la Akheri hadi Usa River. Hatutaraji kuleta watu kutoka Arusha au Hai kama wenzetu (Chadema), sisi tutakuwa na watu wa Arumeru na watajaa uwanjani.”


No comments: